KHADIJA MKE WA MTUME 2
Anaolewa na Atiyq bin Aidh
Imepokelewa kuwa siku moja vijana wa kabila la Kikureshi walipokuwa wamekaa karibu na Al Kaaba wakizungumza, aliinuka mmoja wao anayeitwa Al Harith akasema:
“Enyi ndugu zangu nimetia nia ya kuowa”.
Mmojawao akamwambia:
“Uamuzi mzuri huo, kwani tokea alipofariki mama yako na baada ya baba yako kuowa mke mwingine umekuwa unaishi peke yako”.
Mwengine akasema:
“Umefanya vizuri kuamua kuoa, kwani kila mwanamke anatamani kuolewa na mtu kama wewe, maana baba yako ni katika watu wanaoheshimika katika kabila la Kikureshi, na wewe unamiliki mali nyingi sana, sidhani kama yupo mwanamke atakayekukataa”.
Al Harith Akawatizama wenzake kwa muda, kisha akasema:
“Nyinyi mnadhania hivyo kwa sababu ni rafiki zangu, lakini mnakosea”.
“Tunakosea vipi? Hebu tufahamishe”.
Akawaambia:
“Nilitaka kumuowa Khadija, lakini baba yake alinikatalia kwa sababu eti anasema kuwa kabila langu ni duni kuliko kabila lake”.
Wenzake wakasema:
“Bila shaka hiyo, kwani Khadija ni binti wa Khuwaylid bin Asad naye ni mtu mtukufu miongoni mwa mabwana wa kabila la Kikureshi mwenye kumiliki mali nyingi sana na nyumba kubwa ambayo daima inapokea wageni mbali mbali wanaokuja Makka”.
Mwengine akasema:
“Na Khadija binti yake ni uwa katika mauwa ya Makka, kwani yeye ni mzuri wa umbo na mbora wa mwenendo na tabia, na sifa zake njema pamoja na hekima na uhodari wa kuyapima mambo katika akili yake, vyote hivyo vinajulikana na kila mtu”.
Walipokuwa katika hali ile alipita mbele yao mtu mrefu, mwingi wa haiba aliyevaa nguo zilizoshonwa vizuri na kupambwa, pamoja na kilemba, na nyuma yake kundi la watu lilikuwa likimfuata.
Watu wote walinyamaza kimya huku wakimtazama mtu huyo alipokuwa akipita, kisha mmoja wao akasema kwa sauti ndogo hafifu:
“Huyu ndiye Khuwaylid baba yake Khadija, na walio nyuma yake ni watu wa kabila lake”.
Mwengine akasema:
“Amekuja kutufu Al Kaaba kama kawaida yake ya kila siku”.
Baada ya kutufu Al Kaaba, Khuwaylid akatafuta mahala karibu na Al Kaaba ili aweze kukaa na kujipumzisha, na alipokuwa katika hali ile, kijana mmoja aliiunuka na kwenda kumkabili.
Kijana huyo alikuwa mwenye sura na umbile la kupendeza ambaye kutokana na vazi lake alionyesha kuwa ni mtu tajiri sana, na nyuma yake pia kundi la watu lilikuwa likimfuata kwa heshima na adabu.
Mtu huyo alikuwa ni Atiq bin Aidh, mmoja katika watu wanaoheshimika miongoni mwa matajiri wakubwa wa kabila la Kikureshi.anayetokana na kabila la Bani Makhzum.
Mmoja katika wale vijana akasema:
“Mtizameni vizuri! Mtu huyu anapigiwa mifano katika ushujaa na ukarimu”.
Baada ya kumkabili Khuwaylid bin Asad, Atiq akamwambia:
“Asubuhi njema ewe Khuwaylid”.
Khuwaylid akamjibu:
“Njema kwako pia ewe Atiq”.
Atiq:
“Nimekuja kwa ajili ya mazungumzo na wewe ewe mwana wa ami yangu, lakini mazungumzo yenyewe hayafai kuzungumzwa hapa penye Al Kaaba mbele ya watu”.
Khuwaylid akamwambia:
“Karibu nyumbani kwangu”.
Siku ya pili yake Atiq akamwendea nyumbani kwake na kumwambia:
“Nimekuja kumposa binti yako ewe bin ami yangu”.
Khuwaylid akamuuliza:
“Umekuja kumposa Khadija au Hala?”
“Bali nimekuja kumposa Khadija ewe bin ami yangu”.
“Vyema, lakini itabidi kwanza nimuulize Khadija mwenyewe ili nijuwe rai yake."
Atiq akasema kwa mshangao:
“Lakini wewe ni baba yake na unanijuwa mimi vizuri na unaijuwa daraja yangu katika kabila la Kikureshi pamoja na mwenendo na tabia zangu”.
Khuwaylid akamjibu:
“Bila shaka ewe bin ami yangu natambuwa yote hayo, natambua vizuri pia kuwa anakustahikia mwanamke yeyote wa Kikureshi, isipokuwa mimi siwezi kuamua lolote juu ya Khadija mpaka kwanza nimuulize mwenyewe na aridhike.”
Atiq akaondoka huku akisema kumwambia Khuwaylid:
“Vyema, fanya hivyo na mimi nitasubiri”.
Baada ya Atiq kuondoka, Khuwaylid akaingia kwa binti yake Khadija na kumjulisha juu ya Atiq, akamwambia:
“Ewe Khadija, kwa hakika Atiq amekuja kukuposa, nini rai yako?”
Khadija akasema kumwambia babake:
“Nini rai yako wewe kwanza ewe baba yangu?”
Baba yake akamwambia:
“Yeye ni bwana katika mabwana wa Kabila la Bani Makhzum na ana mali nyingi sana”.
Bibi Khadija akasema:
“Baba yangu, mimi sikuulizi juu ya sifa hizo, bali nataka kujuwa juu ya sifa zake nyingine kama vile ushujaa na ukarimu na kwamba hawafanyii ubakhili wenye kuhitaji wanapomwendea.”
Baba yake akamwambia:
“Atiq bin Aaidh yuko kama ulivyosema ewe Khadija. Yeye ni shujaa, mkarimu anayependa wageni. Hakika sifa zote unazozitafuta anazo mwanamume huyu”.
Bibi Khadija akasema:
“Basi, ikiwa ni hivyo fanya vile unavyoona wewe kuwa ni sawa ewe baba yangu”.
Bibi Khadija (Radhiya Llahuu anha) akaolewa na Atiq wakapata mtoto waliyempa jina la Hind, na wakaishi kwa wema mpaka alipofariki mumewe jambo lililomfanya Bi Khadija awe na huzuni kubwa
No comments