KHADIJA MKE WA MTUME 4



Baada ya kupatwa na misiba miwili hiyo, (kufiwa na mumewe wa pili na kufiwa na baba yake) Bibi Khadija (Radhiya Llahu anha) aliishi akiwa mwingi wa huzuni na mwingi wa kutafakari. alijitenga mbali na watu na aliacha hata kwenda kutufu Al Kaaba kama alivyokuwa akifanya hapo mwanzo.
Inajulikana kuwa Bibi Khadija (Radhiya Llahu anha) hakupata hata siku moja kuyasujudia masanamu yaliyokuwepo hapo, na hii ni siri aliyomjulisha bin ami yake maarufu Waraqah bin Noufel aliyekuwa akifuata dini ya Manasara.
Waraqah bin Noufel huyu alikuwa mcha Mungu sana na alikuwa akisoma sana vitabu vilivyotangulia na kwa ajili hiyo alikuwa akijulikana sana miongoni mwa waarabu wa Makka kwa ucha Mungu wake na wema wake.

Siku moja Bibi Khadija (Radhiya Llahu anha) akiwa na uso uliojaa huzuni alikwenda kumtembelea bin ami yake huyo aliyemuuliza:
“Kuna nini binti ami yangu, mbona nakuona una huzuni nyingi?”
Bibi Khadija akamwambia:
“Sijaiona tena furaha tokea alipofariki baba yangu, na mali nyingi niliyoirithi haikuweza kuziba pengo lake”.
Waraqah akamwambia:
“Usihuzunike ewe binti ami yangu, utakuja kuonana naye Akhera”.
Bibi Khadija akashangaa:
“Akhera? Ni kitu gani hicho kinachoitwa akhera ewe bin ami yangu?”
Waraqah:
“Hayo ni maisha baada ya kifo, na katika maisha hayo kila nafsi itapata jaza yake kutokana na yale yaliyotanguliza mikono yake”.
Bibi Khadija akauliza huku akitetemeka:
“Ina maana kuwa baba yangu hivi sasa yuhai?”
Waraqah akamwambia:
“Ndiyo, roho yake iko hai, isipokuwa mwili wake ushachanganyika na udongo wa ardhi”.
Bibi Khadija akaanza kusema huku mwili wake ukiwa unamtetemeka:
“Bin ami yangu, nataka kukupa siri niliyoizuwia moyoni mwangu tokea nilipokuwa mtoto mdogo mwenye umri wa miaka sita”.
Waraqah akasema:
“Sema ewe binti ami yangu wala usiwe na khofu”.
Bibi Khadija (Radhiya Llahu anha) akasema:
“Nilipokuwa na umri wa miaka sita hivi, nilikwenda siku moja pamoja na baba yangu penye Al Kaaba nikamuona akisimama mbele ya masanamu yaliyotengenezwa kwa mawe kisha anayakabili na kukiinamisha kichwa chake kwa kuyaheshimu. Nikamuuliza:
“Nini haya masanamu ewe baba yangu?”
Akaniambia:
“Hii ni miungu tunayoiabudu”.
Nikashangazwa nikiwa bado mdogo, vipi watu wanayaabudu mawe yasiyoweza kudhuru wala kunufaisha?”
Waraqah akamtizama Bibi Khadija (Radhiya Llahu anha) huku akitabasamu, kisha akamwambia:
“Uliwahi kumhadithia mtu yeyote katika watu wa nyumbani?”
Bibi Khadija akasema:
“Abadan, abadan. Sijapata kumhadithia mtu yeyote, kwani nilikuwa nikiogopa sana, nikaificha siri hii mpaka nilipokuja kukuhadithia wewe sasa hivi. Nini rai yako ewe bin ami yangu?”
Waraqah akamwambia:
“Huo ndio ukweli wenyewe. Yale ni mawe tu yasiyodhuru wala kunufaisha. Na atatokea katika zama zetu hizi Mtume anayesubiriwa atakayeyavunja masanamu haya na kuondoa ushirikina na uonevu katika ardhi”.
Bibi Khadija (Radhiya Llahuu anha) akauliza:
“Na lini atakuja Mtume huyo?”
Waraqah akasema:
“Mwenyezi Mungu ndiye Anayejuwa zaidi, isipokuwa vitabu vinasema kuwa; atatokea Mtume katika wakati huu wetu na yeye ndiye atakayekuwa mwisho wa mitume”.
Bibi Khadija akauliza:
“Na katika kundi lipi atatokea mtume huyo?”
Waraqah akasema:
“Allahu aalam, lakini Mayahudi wanasema kuwa atakuwa katika wao, na vitabu vinasema kuwa atakuwa miongoni mwa Waarabu”.
Bibi Khadija:
“Na uliyajuaje yote haya ewe bin ami yangu?”
Waraqah:
“Haya yameandikwa katika Tuarati kitabu cha Mayahudi na katika Injili kitabu cha Manasara”.

Bibi Khadija akaondoka hapo huku mawazo yake yote yakiwa juu ya huyo Mtume mpya aliyebashiriwa na bin ami yake atakayeuondoa ushirikina na dhulma na jeuri iliyopindukia mipaka, lakini wakati huo huo mazungumzo hayo yalimsaidia sana katika kupunguza uzito uliokuwepo kifuani pake na huzuni aliyokuwa nayo, na kwa ajili hiyo akaanza tena kufanya shughuli zake za kawaida pamoja na za kibiashara.

No comments

Powered by Blogger.